Dunia inabadilika kwa kasi na kwa namna mbalimbali, imefikia kipindi mabadiliko yamekuwa ni kitu kisichoepukika, mtu aweza kubadilika na kuwa mzuri zaidi au mbaya zaidi ya alivyokuwa mwanzo. Lengo la somo hili ni kuhamasiha mabadiliko yanayomfanya mtu awe mzuri zaidi na kupinga mabadiliko yanayomfanya mtu awe mbaya. Kwa sababu lengo ni kuleta mabadiliko katika maisha ya watu, ndo maana sura hii ya kwanza inazungumzia mabadiliko. Kuna watu wahabadiliki kwa sababu tu rahisi ya kutokujua umuhimu wa mabadiliko na jinsi ya kuchukua hatua zinazoweza kuleta mabadiliko katika maisha yao. Ni maombi yangu na dua kwamba Mungu atumie somo hili kubadilisha maisha ya watu wengi.
Tunapozungumzia mabadiliko tunamaanisha kukua, kuongezeka, kuendelea kutoka hali moja kwenda nyingine, kiwango kimoja kwenda kingine, kuacha kufanya kitu kimoja na kuanza kufanya kitu kingine, kuendelea kufanya kitu kile kile lakini kwa ubora zaidi. Inaweza kumaanisha pia kuondoa kitu kimoja mahali fulani na kuleta kitu kingine mfano kuacha tabia fulani isiyo na manufaa na kujenga tabia nyingine yenye manufaa. Neno lenye nguvu zaidi ni mageuzi, mtu unageuzwa na kuwa mtu mwingine kiroho na kitabia, kifamilia, kiuchumi na katika mambo mengine yote yahusuyo maisha kwa ujumla.
Neno la Mungu limezungumzia sana kuhusu mabadiliko na lengo hasa la Mungu ni kubadilisha maisha ya watu. Nami kama mshirika au mdau mkuu wa ufalme wa Mungu sina budi kushiriki kikamilifu katika mpango wa Mungu wa kubadilisha maisha ya watu. Hakika baada ya kusoma utakuwa mtu mwingine kabisa.
Biblia inasema habari za Yesu Kristo katika Luka 2:52 Naye Yesu akakua katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.
Neno la Mungu linasema katikaYohana 14 Mbegu ikikaa hivyo hivyo huwa haizai, lakini ikifa huzaa sana. Ukiendelea kufanya mamyo yaleyale kwa jinsi ileile utapa matokeo yaleyale, kitendo cha mbegu kufa ni kwamba inabadilika kutoka hali moja kwenda nyingine na ndipo inapoaanza kuzaa sana, wengi wetu hatuzai sana kama Yesu alivyosema katika Yohana 15:2 kwa sababu tuko katika hali ileile tumekaa vivyo hivyo.
Ukitaka vitu ambavyo hujawahi kuwa navyo, lazima ufanye mambo ambayo hujawahi kuyafanya. Ni wale tu wenye hekima kupita kiasi na wajinga kupita kiasi hubaki vile vile wakipinga mabadiliko ya kila namna.
Kuvua tabia zisizofaa na kuvaa tabia zinazofaa
Warumi 12:2 Mgeuzwe nia (mawazo, mitazamo, fikra) zenu kwa kufanywa upya
Wakolosai 3:5 – 10, (5) Kwa hiyo, kiueni kabisa cho chote kilicho ndani yenu cha asili ya kidunia: Yaani, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya na kutamani, ambayo ndiyo ibada ya sanamu. (6) Kwa sababu ya mambo haya, ghadhabu ya Mungu inakuja. ( 7) Ninyi pia zamani mlienenda katika mambo haya mlipoishi maisha hayo. (8 ) Lakini sasa yawekeni mbali nanyi mambo kama haya yote, yaani : Hasira, ghadhabu, uovu, masingizio na lugha chafu kutoka midomoni mwenu. (9)Msiambiane uongo kwa maana mmevua kabisa utu wenu wa kale pamoja na matendo yake (10)nanyi mmevaa utu mpya unaofanywa upya katika ufahamu sawasawa na mfano wa Mwumba wake.
Waefeso 4: 21-24, (21) Kama hivyo ndivyo ilivyo, ninyi mmemsikia, tena mmefundishwa naye, vile kweli ilivyo katika Yesu. 22Mlifundishwa kuuvua mwenendo wenu wa zamani, utu wenu wa kale, ulioharibiwa na tamaa zake za udanganyifu. 23Mfanywe upya roho ya nia zenu, 24mkajivike utu mpya, ulioumbwa sawa sawa na mfano wa Mungu katika haki yote na utakatifu.
Hapa mtumishi wa Mungu Paulo anazungumza kwa habari ya kuvua na kuvaa. Unavua tabia zisizofaa na unavaa tabia zinazofaa. Unavua mitazamo isiyofaa na unavaa mitazamo inyofaa. Kuvua hapa anamaanisha kuacha jambo fulani na kuvaa anamaanisha kuanza kufanya jambo jingine. Mfano una tabia ya kutokuweka akiba ya kutosha unavua tabia hiyo na unavaa tabia ya kuweka akiba au kuwekeza ili upate zaidi, unaangalie mbele zaidi ya hapo ulipo na matokea yake kubadilika na kuwa mtu tofauti na ulivyokuwa mwanzo. Lengo hasa la kila mtu halina sababu ya kuwa kitu kingine kinyume na mapenzi ya Mungu, ni muhimu sana kuhakikiksha kuwa tunayajua mapenzi ya Mungu kwetu na mabadiliko yoyote sharti yalenge kuwa kama Mungu anavyotaka tuwe, kwani kuwa tofaouti na Mungu anavyotaka hakuna furaha na utoshelevu wa maisha hata kama utakuwa na mali nyingi kiasi gani. Mtume Paulo anasema katika Waefeso 5: 17 Kwa hiyo msiwe wajinga, bali mpate kujua nini yaliyo mapenzi ya Bwana. Huu ni mstari wa msingi sana katika somo hili. Lengo hasa ni kukuwezesha wewe uyafahamu mapenzi ya Mungu na uenende na kuishi katika hayo.
Kutimiza makusudi ya Mungu katika maisha yako siyo kitu kinachotokea tu hivi hivi, unachokiusubiri ukiwa umebweteka, inahitaji uamuzi, kuchukua hatua ambazo wakati mwingine hujawahi kuzichukua kabisa, kubadilisha tabia fulani fulani zinazokukandamiza, kubadilisha usemi wako, maombi yako, matumizi ya muda, marafiki zako na wakati mwingine hata watu unaoambatana nao mara kwa mara kwani wana nguvu ya kukuambukiza tabia njema au mbaya. Mtu mwenye hekima aliyeamua kutembea na kuishi katika mapenzi ya Mungu huchagua marafiki kwa uangalifu mkubwa.
Mabadiliko ya kweli hutokea pale ambapo kanuni za mafanikio zinafanyika kuwa tabia za watu na si misemo ya kufikirika na kuzungumzika tu. Uadilifu, uaminifu, uvimilivu, uotaji, nk. Vinakuwa ni tabia yako, ni sehemu ya maisha yako.
–Cosmas Kisela