Imani-III

Katika sehemu iliyopita tuliangalia tofauti kati ya Imani na Tumaini. Katika sehemu hii ya Tatu [III] ya somo letu tutaangalia Tabia za Imani. Tabia hizi za Imani, katika utendaji kazi wake, hubadilika kutokana na sababu mbali mbali kama vile mazingira, ugumu wa tatizo lililoko mbele, kusudi linalokusudiwa nk.

Aina za tabia za imani katika utendaji kazi wake ni hizi zifuatazo:

1.Huona yasiyoonekana

Mungu aliona ya ulimwengu ndani yake hata kabla hajatamka. Alimuona mwanadamu  kabla hajamuumba. Mwanzo 1:27 inasema Mungu alimuumba mtu kwa mfano wake mwenyewe. Alikuwa na picha ya mtu kisha akamuumba kwa kufuata  au ile ramani Paulo aliandika.

Biblia inasema, tusiviangalie vinavyoonekana bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu, bali visivyoonekana ni vya milele. 2Kor 4:18.

Kwa maana twaenenda kwa Imani si kwa kuona. 2Kor 5:7. Paulo anaweka mkazo kuwa mwamini hapaswi kutawaliwa na yale anayoona katika ulimwengu wa asili. Hivyo kuona yasiyoonekana ni moja ya utendani kazi wa Imani.

2.Huona kabla haijatenda

Watu wengi hujaribu kuongea Imani kabla hawajawa na taswira ya kitu ndani ya roho zao kwanza . Kwa sababu hawajauona huo uhalisi kile wanachosema hakiwezi kutimia. Kisha wanasema kuwa kukiri Imani hakutendi kazi, nimeshakiri kwamba nimeponywa lakini bado ninaumwa. Kama bado wanaumwa ni kwa sababu bila shaka hawakuwa wameumbiwa ndani yao taswira ya kujiona wazima kwanza maana aonavyo mtu nafsini mwake ndivyo alivyo. Mithali 23:7

Wakati akielezea hali katika siku za mwisho, Yesu alisema kuwa mioyo ya wanadamu itavunjika kwa sababu ya hofu ya kile kinachoujilia ulimwengu. Luka 21:26. Usemi  huu kwa kawaida unamaanisha kuwa roho za watu ambao hawaishi kwa Imani zitashindwa kuzaa matunda. Ukiri ni muhimu lakini ni sehemu tu ya mduara mzima wa Imani.

3.Hukamilisha kazi

Baada ya kusema taswira unayoona Imani husababisha msukumo wa kuanza kutenda kulingana na taswira hiyo. Petro alijiona katika taswira yake akishuka kutoka kwenye mashua na kutembea juu ya maji kumwendea Yesu. Kilichofuatia ile taswira ni maneno aliyoyasema “ Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji. Mathayo 14:28.

Yesu aliposema njoo, Petro alianza kutembea juu ya maji. Imani ya Petro iliona, ikanena na ikatenda lakini aliyaruhusu mazingira kubadili taswira yake. Alipoyaondoa macho yake kutoka kwa yasiyoonekana na kuyaelekeza kwa yanayoonekana hapo hapo akaanza kuzama. Mazingira yanapokuwa kinyume nawe unatakiwa uwe jasiri, katika Imani, kwa matendo na kutumnia kile ninachoita Imani ya kung’oa dari.

Hebu tuangalie mfano wa huu katika Biblia, kwenye Luka 5:18-20, ambapo inatuambia juu ya watu wane waliompeleka rafiki yao mgonjwa kwa Yesu ili akaponywe. Baada ya kupokea taswira ya kumfikisha rafiki yao kwa Yesu, walifunga safari wakiwa wamembeba yule mtu kwenye machela. Walipolifikia lile jengo ambamo Yesu alikuwa akihubiri walikuta limefurika watu na hivyo hawakuweza kuingia ndani. Kuna wakati haya mambo ya Imani yanatenda kazi hapo hapo na wakati mwingine hayatendi! Walijitahidi wawezavyo lakini walishindwa kuingia ndani. Walipoona hivyo wakatafuta njia tofauti ya kumpeleka ndani: Walipanda juu ya dari wakampitisha katika matofali ya juu, wakamshusha yeye na kitanda chake katikati mbele ya Yesu. [Lk 5:19].  Hawakuyaangalia mazingira; Imani yao iliona, ikanena kisha ikatenda!

Watu hao walikuwa majasiri na Imani yao, wakalibomoa dari ili wamfikishe rafiki yao mgonjwa kwa Yesu. Naye Yesu alipoiona Imani yao, alimwambia yule mgonjwa, Ee rafiki, umesamehewa dhambi zako. Yesu alipoiona Imani yao na matendo yake [ya Imani]  alimponya yule mtu.

Imani inatakiwa kutenda kazi namna hii katika maisha yako. Pale unapoona taswira, usiruhusu chochote kikuzuie. Anza kusema kisha Fanya kitendo, na ukikutana na jambo ambalo ni kama vile linakwamisha wewe ufikie taswira uliyoiona moyoni mwako: Tumia Imani ya aina hii ya kung’oa dari kutafuta mlango. Wakati ukielekea kwenye taswira uliyoiona moyoni mwako na ukakutana na mlango uliofungwa, usikate tamaa. Endelea kubisha hadi utakapofunguliwa! Ni hakika Yesu ataiona imani yako na kukutana na hitaji lako.

4.Husimama

Ni lazima  ukusudie kushinda. Unaposema “Nitajaribu” unamwambia Ibilisi kuwa una nafasi nusu-nusu ya kushinda au kushindwa; yaani ni kubahatisha tu. Usijaribu kuishi kwa Imani bali Fanya kabisa. Achana na mipango ya kimwili.

- Basi ndugu zangu nawaarifu ile injili niliyowahubiri ambayo ndiyo mliyoipokea na katika hiyo mnasimama. 1Kor 15:1

-Simamia ile injili mliyoipokea. Simama imara katika Imani. Fanya kiume, ukawe hodari. 1Kor 16:13. Imani husimama, kwa maana nyingine hudumu!

Hatuwezi kufanana na watu wa dunia wanaotegemea mambo ya kawaida ya mwili wanaposhikwa na shinikizo na maadui wakiwaambia hakuna namna ya kujinasua. Watu hawa huwa hawana nguvu.

Mfano: Mtume Paulo alisema, huku akiwa na uhakika kwamba Mungu anaweza kufanya yale aliyoahidi [Warumi 4:21], “Nina uhakika kuwa mtatembea kwa Imani na si kwa kuona [1Kor 5:7] kwa maana ninamjua yeye niliyemwamini. [2Tim 1:12]. Mtume Paulo alikuwa mtu wa uhakika, jasiri na mwenye kujiamini katika Imani na nguvu.

Baadhi ya watu wanadhani kuwa maisha ya Imani ni kuishi kwa njia ya kujihatarisha. Watu ambao hawajiamini ni wale ambao hawalijuwi neno  lake Mungu. Mungu anasema ‘Mimi sitalihalifu agano langu, sitalibadli neno lililotoka mdomoni mwangu [Zaburi 89:34]. Na Mungu si mwongo.

Mfano mwingine: Unapomuona mtu tajiri ambaye ana magari na majumba, kwa akili ni rahisi kusema bila shaka mtu huyo atanipatia pesa nifanye Huduma au kujenga Kanisa. Na hapo ndipo Mungu atakunja mikono yake mpaka utakapoacha kuingilia sehemu inayomhusu yeye. Unapoamua kusema BWANA, NINAKUTWIKA FADHAA ZANGU  ZOTE!, ndipo Mungu husema ‘hicho ndicho nilichokuwa nakisubiri’. Anaamua kuchukua sehemu yake na kuleta madhihirisho kwa njia za kushangaza kabisa.

Katika sehemu inayofuata tutaangalia tabia zaidi za Imani katika utendaji kazi wake!

Mwinjilisti David Kimwaga

IMANI – II

Mwinjilist David Kimwaga

Katika sehemu ya kwanza ya somo hili la IMANI tuliangalia mambo mawili ambayo ni Maana ya Imani na Kipimo cha Imani. Leo tunaendelea na somo letu kwa kuangalia kipengere cha tatu, katika mtiririko wa somo hili, abacho ni:

3. TOFAUTI KATI YA IMANI NA TUMAINI

Watu wengi katika Kanisa hufikiria kwamba IMANI na TUMAINI ni kitu kimoja, jambo ambalo si kweli kabisa. Na wako wengi ambao huchanganya matumizi ya Tumaini wakidhani ndiyo matumizi ya Imani, na matumizi ya Imani wakidhani ndiyo matumizi ya Tumaini. Naomba tufuatane katika somo hili na ninaamini kama utafuatilia kwa makini, mwisho wa somo hili utaelewa tofauti kati ya Imani na Tumaini.

Tuanze kuangalia tofauti hizi kwa kuanzia na IMANI:

Katika kitabu kile cha Marko 9:33 imeandikwa: “Yesu akamwabia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye! Kwa nini Yesu anasema ‘Kwake aaminiye’? Ina maana Mungu huwa anajibu Imani. Mungu huwa hajibu Maombi tu bali anajibu Maombi yenye Imani. Hii ndiyo sababu Yesu alisema maneno yafuatayo: Yote yawezekana kwake aaminiye. Maana nyingine ya maneno haya ni Yote hayawezekani kwake asiyeamini.

Katika Marko 9:14-28 tunapata habari ya mtu aliyekuwa anasumbuliwa na pepo na ambaye wanafunzi wa Yesu walishindwa kumuondolea pepo wale. Wanafunzi wa Yesu walishindwa kumtoa kwa sababu hawakuwa na Imani. Biblia inasema ‘Mwenye haki wangu ataishi kwa Imani’. Kwa hiyo unapoomba Mungu ni lazima uamini ndipo Mungu hujibu.

Sasa tuangalie TUMAINI:

Mtu anapoomba jambo lolote na kusema kwamba siku moja atapata tu, hapo siyo Imani tena bali hilo ni Tumaini. Tumaini ni hali ya kutegemea jambo fulani litokee.

Kwa mfano Yesu alisema:

-Atarudi kutuchukua, hilo ni Tumaini letu na tunamsubiri, atakuja.

-Tutafanana naye, hili nalo ni Tumaini.

-Tutatawala naye, hili pia ni tumani letu.

Vile vile tunatumaini juu ya mambo mengi yanayotuhusu ambayo Yesu aliyaahidi. Mifano michache ni katika Yohana 12:26 na Yohana 17:24 .

Mtu hawezi kuchukua vitu ambavyo shetani amevizuia kwa kutumia Tumaini. Kuna watu wengi wanaomba sana lakini wakati wanaomba hujisemea ‘siku moja nitapata!’ Maneno hayo hapo si mahali pake maana kusema hivyo ni kutumainia –Tumani na si kuamini, yaani Imani. Yesu Kristo alipokuwa akiponya watu aliwaambia walioponywa kwamba Imani yako imekuponya, imekutakasa, imekuokoka nk:

- Mwanamke mwenye kutokwa na damu, Marko 5:43;

- Kipofu aliyekaa kando ya njia akiomba sadaka [omba omba], Luka 18:42;

- Mmoja wa wale wakoma kumi, Luka 17:19

Katika Marko 5:25-33 tunasoma habari ya mwanamke aliyekuwa na tatizo lwa kutokwa na damu kwa muda wa miaka kumi na miwili na aliyekuwa amehangaika huku na kule akitafuta kupona. Baada ya kusikia habari za Yesu aliamua moyoni mwake na kusema ‘nikigusa tu vazi la Yesu nitapona!’. Hakusema ‘nikigusa tu vazi ya Yesu nitakuja kupona’ au ‘nitapona pole pole’. Na baada ya kupona Yesu akamwambia ‘Imani yako imekuponya’. Hapa tunaona kwamba Imani ndiyo ilimponya na wala si Tumaini.

Katika mambo yako yanayokusumbua ufumbuzi unao mwenyewe. Pengine umeteseka kumbe ni kwa sababu ya kutojua tofauti kati ya Imani ana Tumaini. Na Imani huja kwa kusikia Neno la Mungu. Ndiyo maana Mungu alitupatia masikio ili tusikie. Imani haiji kwa kusema sana au kwa kuomba sana bali huja kwa kulisikia Neno la Mungu.

Sikiliza sana Neno la Mungu maana kwa kufanya hivyo ndipo Imani itakapokuja. Na Imani ikishakuja hutaweza tena kuichanganya matumizi yake na Tumaini kwa kuwa kinachofanya maombi yajibiwe ni IMANI na wala si TUMAINI. Na pia ni Imani ndiyo inatufanya tumpendeze Mungu.

Somo litaendelea……

IMANI – I

Mwinjilisti David Kimwaga

UTANGULIZI

Kwanza ninamshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuandaa somo hili. Ni matumaini yangu kwamba katika kulisoma utapata kitu cha kuongezea katika yale unayoyafahamu na/au kupata mapya kuhusu IMANI. Amina!

1. IMANI NI NINI?

Katika kile kitabu cha Waraka kwa Waebrania, sura ya 11:1, tunapata tafsiri ya imani ambayo nafikiri karibu kila mkristo anaifahamu. Andiko hilo linasema hivi;

“Basi imani ni kuwa na uhakika wa mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana”.

Tukiendelea mbele katika kusoma maandiko tunakuja kuona kuwa:

Imani ni njia ya kumpendeza Mungu.

Katika Ebrania 11:6 kwamba “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza”. Ina maana kuna watu wapo hata sasa, ambao ni wakristo, lakini hawampendezi Mungu. Kutokumpendeza Mungu kwa lugha nyingine ni kumdharau Mungu kwamba hawezi kufanya mambo yako.

-Imani ni njia ya ushindi wetu kwa kila kitu ambacho shetani anakirusha kwetu, katika mapito yote kwenye maisha.

Katika 1Yohana 5:4 Biblia inasema ‘Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu, na huku ndiko kuushinda ulimwengu, yaani hiyo Imani yetu’. Tukitafakati maneno haya tunaweza kuona kuwa kila mtu, yaani ye yote, aliyezaliwa na Mungu ana uwezo wa kuushinda ulimwengu. Lakini ambaye hajazaliwa naye hawezi kuushinda ulimwengu. Kuushinda ulimwengu ni kuyashinda ya ulimwengu.

Kitu kinachomfanya aliyezaliwa na Mungu aushinde ulimwengu ni kwa sababu ana Asili ya Mungu. Yohana 16:33. Adamu alipouuwa u-asili wa Mungu ndani yake Yesu Kristo aliuhuisha ukawa Hai.

-Mungu anatuagiza tuishi kwa Imani. Rumi 1:17 inasema mwenye haki wangu ataishi kwa Imani.

-Maisha ya Imani ni ya matukio yasiyo ya kawaida ya ushindi.

2. KIPIMO CHA IMANI

Katika kitabu cha Waraka wa mtume Paulo kwa Warumi, sura ile ya 12 tunapata maneno haya:

“Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii, bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu. Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunai, bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha Imani” Rumi 12:1-3

Na katika kitabu kile cha Waraka wa Pili wa mtume Paulo kwa Wathesalonike sura ile ya 3 kuna maneno haya:

“Hatimaye, ndugu, tuombeeni, neno la Bwana liendelee, na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu; tukaokolewe na watu wasio haki, wabaya; maana si wote walio na imani” 2Thes 3:1-2.

Kuna baadhi ya watu wanachanganywa na haya maandiko mawili, wanasema, katika Warumi 12:3 andiko linasema kila mmoja kapewa Imani, halafu katika 2Thes 3:2 andiko linasema kuna baadhi ya watu hawana Imani. Ukisoma kwa haraka haraka ni kama vile maandiko yanapingana. Lakini kwa kuandika hivi, mtume Paulo alimaanisha nini? Jibu lake ni rahisi wakati utakapoligawa Neno la Mungu kwa usahihi. Katika ile Warumi 12, wakati mtume Paulo aliposema Mungu amemgawia kila mtu kipimo cha Imani, anazungumzia juu ya Kanisa. Anasema ‘basi ndugu zangu…’ na ‘namwambia kila mtu aliyeko kwenu’, yaani hao ndugu. Na katika ile 2Thes 3, wakati mtume Paulo anaposema ‘maana si wote walio na imani…’ anazungumzia juu ya watu waovu wa duniani, siyo Kanisa. Watu waliomo kanisani wamepewa Imani, watu wa dunia hawana. Kugawiwa kipimo cha Imani ni lazima uzaliwe mara ya pili. Waefeso 2:8-9 inasema ‘Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya Imani, ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.

Kama umemfuata Yesu Kristo kama Bwana maishani mwako, manaeno haya ‘kila mtu aliye kati yenu…..’ yanakuhusisha na wewe. Mungu amekupa wewe Imani katika kipimo fulani.

Kama Mungu anawapa baadhi ya watu kipimo kikubwa zaidi cha Imani kuliko wengine, ni kigezo gani basi anachotumia Kuamua ni nani apate na kwa kiasi gani? Na ni kwa njia gani tutamsisimua Mungu kiasi cha kutosha ili atupatie sisi Imani zaidi?

Imani ni kipawa cha Mungu sio kwa matendo mtu awaye yote asije akajisifu. Biblia inasema kuwa Mungu ni wa haki na wala hana upendeleo. (Matendo 10:34). Humgawia kila mwamini kipimo kile kile cha Imani.

Mfano: Unapokuwa umealika watu nyumbani kwako kwa ajili ya keki, huwezi kumpa mtu mmoja keki yote, bali utampa kila mtu kiasi chake; na kila mtu angepata kiasi kile kile, kipimo kilichokusudiwa.

-Mungu alitangulia kuweka kipimo cha Imani ambacho kila mtu anapozaliwa mara ya pili tu anakuta kipimo hicho kinamsubiri. Kwa maneno mengine mtu anapookoka tu anapokea imani. Alitoa kwa kila mwamini fungu lililokusudiwa. Kipimo kilichotolewa kutoka kwenye Imani yake mwenyewe.

-Yesu alisema ‘Mwaminini Mungu’.(Marko 11:22). Tafsiri nyingine zinasema ‘Iweni na imani ya Mungu’ au ‘Iweni na Imani kama ya Mungu. Nina hakika, kwamba, kipimo cha Imani ambacho Mungu anamgawia kila mwamini ni cha ile ile Imani ya ki-Mungu mwenyewe.

-Kipimo hicho cha Imani ni cha aina ile ile ambayo iliumba ulimwengu; Ndiyo iliyowaongoza wana wa Israel milioni tatu kutoka kwenye utumwa katika nchi ya Misri na ikawafanyia njia kavu katika Bahari ya Shamu. Ndiyo iliyomfufua Yesu kutoka kwa wafu na imetenda kazi katika maisha ya watu wakuu wa Imani katika vizazi vyote!

Somo litaendelea……

Pamoja na kuhubiri Injili na kufundisha Neno la Mungu ninafanya pia Huduma ya maombezi kwa njia ya simu. Popote pale ulipo, tatizo lolote linalokusumbua, kama unaamini Mungu anaweza kufanya jambo kupitia Jina la Yesu Kristo, piga simu wakati wowote.

Piga simu namba +255 712 180392.