
Msichana jasiri anayempenda Mungu ni Yule anayeweza WAKATI WOTE kujizuia ulimi wake (Yakobo 3:1-11 soma yote), Yakobo 3:2, “Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na ulimi wake wote kama kwa lijamu.” Inapendeza sana binti kujichunga usemi wake na kuhakikisha kila usemi unaendana kama yeye alivyo kama msichana aliyeokoka, Mathayo 12:35-37, ” Mtu mwema katika akiba njema hutoa mema, na mtu mbaya katika akiba mbaya hutoa mabaya.” kila mtu atatoa hesabu ya maneno yake. Huwezi kuzipata Baraka za Mungu ikiwa kinywa hicho hicho huzungumza mabaya. Wakolosai 3:8, “lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, ghadhabu, na uovu, na matukano na matusi vinywani mwenu.”
Tuweni makini na vinywa vyetu, mazungumzo yetu hufanyika Baraka ama laana katika maisha yetu. Zaburi 141:3 “Ee Bwana uweke mlinzi kinywani pangu, mngojezi mlangoni pa midomo yangu” Mithali 16:23-24, “Moyo wa mwenye hekima hufundisha kinywa chake, huzidisha elimu ya midomo yake, Maneno yapendezayo ni kama sega la asali, ni tamu nafsini, na afya mifupani ”
1. Wadada waliookoka, jihadhari kuongea maneno yenye sumu au kuropoka hasa wakati wa hasira. Fikiria kwanza kabla hujajibu lolote Yakobo 1:19, “Hayo mnajua, ndugu zangu wapenzi. Basi kila mtu na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema, wala kukasirika ” Mithali 17:27-28, “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa , na mwenye roho ya utulivu ana busara, Hata mpumbavu akinyamaza, huhesabiwa hekima, Akifumba mdomo wake huhesabiwa ufahamu ” 1Wathesalonike 4:11 ” Tena mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza” Ni muhimu mabinti kutambua mahali gani yakupasa kuzungumza na wapi uwe kimya, kwa kufanya hivyo hutampa shetani nafasi ya kutaka wewe uzungumze yasiyofaa yatakayouharibu mwili wa Kristo.
2. Epuka kusengenya, mafarakano na lugha chafu Waefeso 4:31, “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya” Mithali 9:13 “Mwanamke mpumbavu hupiga kelele, Ni mjinga hajui kitu ” Mithali 21:23 ” Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake, Atajilinda nafsi yake na taabu
1 Wakorinto 1:10, ” Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja, wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja” umbea umevunja ndoa za watu, uchumba, marafiki, watumishi kanisani na maofisini wamefarakana kwa sababu ya masengenyo. Kama msichana jisitiri kwa lugha safi iliyojaa upendo au nyamaza kimya. Usiharibu ushuhuda waka kwa sababu ya kinywa chako.
Uongo hautakiwi kwa mabinti. Waefeso 4:25, “Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake, kwa maana tu kiungo kila mmoja cha mwenzake ” Binti aliyeokoka anautumia muda wake vizuri katika kumtumikia Mungu na watu wengine na sio kukaa katika makundi na kuwasema watu, watumishi wa Mungu. 1 Timotheo 5:13-14, “Tena, pamoja na hayo, hujifunza kuwa wavivu, wakizunguka zunguka nyumba kwa nyumba; wala si wavivu tu, lakini ni wachongezi na wadadisi, wakinena maneno yasiyowapasa.
Matendo, usemi wako, na muonekano wako huonesha wazi wewe ni binti wa namna gani jiulize mwenyewe una ushuhuda upi kwa wengine? Neno la Mungu linasema “Sasa basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu” Wengine watakutambua kwa matendo yako au matunda yako.
Binti uliyeokoka UNAMVAA YESU na KUTEMBEA KAMA MWANA WA NURUNI Warumi 13:12-14, “Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia, basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru, Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu, si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu, Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake ”
3. Binti uliyeokoka umejaa upendo kwa Mungu na wenzako . Waefeso 4:15 “ Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo” Upendo husababisha uwafikirie wengine sio wewe kwanza. Husababisha kufikiria mahitaji ya watu kwanza na haki zao. Upendo huwafanya wengine wawe muhimu kuliko wewe.
Muda wako unautumiaje?
Muda ni kitu cha thamani sana sio vizuri binti kuupoteza muda wako kwa mambo yasiyoujenga mwili wa Kristo. Kila mwanadamu anao muda sawa na wa mwenzake awe ameajiriwa au amejiajiri mwenyewe. Awe kijana au mzee, awe tajiri ama masikini. Muda tumegawiwa sawa sawa.
Binti aliyeokoka anaukomboa muda wake. Waefeso 5:16, ” Mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu” Binti anayekwenda na wakati ni Yule anayetumia muda wake kwa hekima na kushughulikia yale yaliyopotea na kuyarejesha. Kama huduma, kazi, utakatifu, kibali n.k. Dunia inapojaribu kuwafanya mabinti kwenda na wakati kwa jinsi isiyofaa binti uliyeokoka wewe fanya yale Mungu anayokuagiza, ufanye yanayomrudishia yeye sifa na UTUKUFU. Wakolosai 4:5, “Upole wenu na ujulikane na watu wote. Bwana yu karibu “
Mungu atahukumu ni kwa jinsi gani umeutumia muda wako. I Petro 1:17, “Na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni ”
Msichana aliyeokoka ni balozi wa Bwana Yesu, tunamuwakilisha Yesu. Ndani ya moyo wako tamani Bwana Yesu aonekane kupitia wewe. Uwe na nidhamu kwa muonekano wako, mazungumzo yako, matendo yako na muda wako! Maisha haya siku moja yatabaki historia, lakini yale uliyofanya kwa ajili ya Bwana Yesu hudumu, uwe mbali na marafiki wa dunia hii. Mungu akubariki BINTI!
-MD-