Mungu tunayemwamini katika Yesu Kristo, ni Mungu wa mipango na makusudi kamili. Tangu vizazi na vizazi tabia hii ya Baba yetu, imejidhihirisha wazi.Baba yetu huyu, ambaye pia, ni Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, hawezi kufanya kitu au kusema kitu, bila ya kuwa na sababu.
Mungu aliumba dunia hii, kwa kusudi kamili, ili ikaliwe na watu isiwe tupu. Mungu aliumba jua, mwezi, sayari na nyota mbali mbali, kwa makusudi kamili, ili viwe ndiyo dalili za majira na siku na miaka na tena iwe ndiyo mianga katika anga la mbingu itie nuru juu ya nchi.
Mungu alimtokea Musa katika kijiti kilichokuwa kikiwaka moto, kwa kusudi kamili, ili apate kuwatoa watu wake, wana wa Israeli kutoka Misri. Mungu alimtoa Mwana wake wa pekee Yesu Kristo, kwa kusudi kamili, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.
Mungu alimwaga Roho wake Mtakatifu juu ya watu wake, kwa kusudi kamili, ili wapate nguvu ya kuwawezesha kuwa mashahidi wa Kristo katika ulimwengu mzima. Ni kweli kabisa ya kwamba, Mungu tunayemwamini katika Yesu Kristo, ni Mungu wa mipango na makusudi kamili. Hafanyi kitu bila ya kuwa na sababu nacho.
Kwa hiyo alipokuwa akisema na watumishi wake, alikuwa na kusudi na ujumbe kamili kwa ajili ya watu wake.
Na aliponiita kwenye utumishi wake alikuwa na mipango na makusudi kamili kwa ajili ya watu wake. Kwa hiyo niliposikia sauti yake ndani ya roho yangu nilipokuwa kwenye mkutano wa ‘Easter Crusade’, Tukuyu, Mbeya Aprili 1987, nilijua hakika ya kuwa kuna jambo la muhimu.
Nilisikia sauti ya Bwana ndani ya roho yangu ikisema; “NATAKA KUSEMA NA WATU WANGU”.
Si kwamba nilisikia sauti kama ya mtu akiongea; hapana; bali kwa uwezo wa Roho wake Mtakatifu, nilisikia sauti hiyo ndani ya roho yangu. Na nilijua hakika ya kuwa hiyo ni sauti ya Bwana wangu na Mwokozi wangu. Hata Yeye alisema kuwa ndiye pekee aliye mchungaji mwema, walio wake anawajua, na wao wanamjua, na sauti yake wanaijua (Yohana 10:1-6).
Mkutano huo wa kiroho ulikuwa umejumuisha watu wa Mikoa mbali mbali na pia watu wa madhehebu mbali mbali. Na Bwana aliposema nami kwamba anataka kusema na watu wake ilikuwa ni mchana wa siku ya pili ya mkutano.
Kwa hiyo baada ya kusikia hivyo, nilitafuta mahali pa faragha katika chumba kimoja; nikapiga magoti, na nikawa tayari kusikia lile ambalo Bwana alikuwa anataka lisikike kwa watu wake.
Maneno aliyoniambia yalihusu juu ya UMOJA WA WATU WAKE. Na waliokuwapo kwenye mkutano huo walipata nafasi ya kusikia kwa muhtasari tu, juu ya Umoja wa watu wa Mungu. Maneno hayo ya Bwana juu ya umoja wetu ni muhimu sana. Na kwa ajili hiyo, Roho wa Bwana ameniongoza kuyaandika kwa undani zaidi, ili watu wengi waweze kuyapata na kuyafanyia kazi.
Jambo ambalo Bwana analiona katikati yetu, katikati ya wakristo, ni kukosa Umoja wa kweli. Na jambo hili linamhuzunisha sana Mungu. Hii ni kwa sababu watu wake ndiyo mwili wake (1Wakorintho 12:27). Kwa hiyo kukiwa na nyufa katika uhusiano wa mkristo na mkristo mwingine, maana yake mwili wake umepata nyufa. Kusudi lake kubwa la kutulinda, kututunza, kutulisha, kututakasa na kutuongoza ni ili atulete mbele za Baba yetu aliye mbinguni, bila waa na wala kunyanzi.
Lakini, hali inayoonekana sasa ni ya kusikitisha. ‘Fellowships’ nyingi hazina umoja na zimetawaliwa na mafarakano. Viongozi wa Kanisa nao pia hawana umoja kila mmoja anafanya mambo yake mwenyewe, ambayo anayaona ni bora kuliko ya mwenzake. Vikundi vingi vya huduma za kikristo havina umoja wa kweli.
Yesu Kristo alituombea umoja. Je! Maombi yake yamejibiwa au bado? Na alikuwa na sababu gani alipokuwa anatuombea? Je! Yesu Kristo alikuwa na mpango wowote aliouandaa juu ya umoja wa mwili wake, ambalo ni Kanisa?
Ni nini chanzo cha mafarakano na kukosa umoja katikati ya watu wa Mungu? Tufanye nini ili tupate kusimama katika umoja wa kweli?
Maswali hayo na mengine yanajibiwa katika somo hili.
Sasa, ngoja niseme jambo moja muhimu:
Mungu huyu tunayemtumika ni Mungu aliye na kusudi kamili, katika kila jambo analolifanya na kulisema. Na kwa mtazamo huu, nakuambia hivi, Mungu ameweka maandiko ya somo hili mikononi mwako kwa kusudi kamili, kwa ajili ya utukufu wa Jina lake Takatifu.
Kwanza: Kwa sababu anakupenda upeo, hapendi upotee.
Pili: Kwa sababu wewe ni kiungo cha mwili wake, ambao ndilo Kanisa
Tatu: Kwa sababu anataka uhusike moja kwa moja katika kushirikiana na Roho wake Mtakatifu, ili kuwashirikisha wengine ujumbe huu.
Ni maombi yangu kwa Mungu katika Jina la Yesu Kristo aliye hai, ya kuwa Roho wake akutie nuru katika utu wako wa ndani upate kuyaelewa yote na kuyafanyia kazi ipasavyo. Na ukiishayasoma uwashirikishe wengine bila kuyapindua pindua.
Hizi ni siku za mwisho, na tunatakiwa tuwe waangalifu katika yote tunayoyasikia au kuyasoma. Tunatakiwa tuyachambue, na kuyapima, halafu tuyachukue yaliyo mema yanayotujenga pamoja na siyo kutubomoa.
Kwa hiyo nakushauri, katika Jina la Yesu Kristo, ya kwamba unapoyasoma yaliyomo humu, uwe na BIBLIA yako karibu upate kuifuatilia mistari yote niliyoinukulu. Bwana na akuwezeshe kuyatafakari na kuyafanyia kazi ili wote tuwe na Umoja kama Baba na Kristo walivyo umoja.
Sifa na Utukufu na uweza, na nguvu vina Mungu wetu katika Kristo Yesu, milele na milele – Amina.
YESU KRISTO ALIOMBA UMOJA KWA AJILI YA NANI?
Neno Umoja maana yake nini?
Yesu Kristo alipokuwa anaomba juu ya Umoja kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Yohana sura ya kumi na Saba, alilitumia neno Umoja mara tano.
Neno Umoja linaweza kuwa na maana mbali mbali, kutokana hasa na mtu anayelitumia, mahali anapolitumia na kwa ajili ya kitu gani.
Neno Umoja likitumika kwa ajili ya watu lina maana ya patana, afikiana, elewana na lingana, katika roho, na nia, mawazo, maneno na matendo.
Yesu Kristo alipokuwa akitumia neno Umoja, alikuwa anamaanisha hao anaowaombea wapatane, waafikiane, waelewane, na walingane katika roho zao, nia zao, mawazo yao, maneno na matendo yao.
Sasa, hili si jambo dogo! Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani, akiwa amevaa mwili wa kibinadamu; kabla ya kufa na kufufuka; aliomba maombi ya namna nyingi. Na mojawapo ya maombi yake kwa Baba Mungu, yalikuwa juu ya Umoja wetu.
“Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao. Wote wawe na Umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja. Mimi ndani yao; nawe ndani yangu, ili wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma, ukawapenda wao kama ulivyonipenda mimi (Yohana 17:20 – 23).
Haya ni maombi yaliyowekwa mikononi mwa Mungu, kwa uzito wa kipekee. Yesu Kristo alipokuwa anaomba maombi haya, alikuwa anajua anaongea na nani, na umuhimu wake ni nini.
Yesu alikuwa anamuombea nani?
Tusipoelewa Yesu Kristo alikuwa anaomba umoja kwa ajili ya nani, hatutaweza kufahamu kwa undani sababu zilizomfanya aombe kwa namna hiyo na kwa wakati huo. Ukizunguka katika vikundi mbali mbali vya watu wa Mungu, utakuta wanasema tuombee umoja. Hili ni jambo muhimu sana, lakini si wote ambao wanafahamu ya kuwa maombi yao ni tofauti na yana lengo lisilofanana na sala ya Bwana Yesu.
Inawezekana hata wewe, umewahi kuomba juu ya umoja. Je huwa unaomba umoja wa watu gani? Au huwa unaomba juu ya umoja wa watu wote? Au huwa unaomba umoja wa madhehebu?
Watu wengi sana wanapoomba juu ya umoja, kwa kusimamia maombi ya Bwana Yesu, huwa wanaomba juu ya umoja wa madhehebu yao.
Lakini nataka ujue, ya kuwa Yesu Kristo alipokuwa anaomba umoja, katika mistari tuliyosoma, alikuwa haombi juu ya umoja wa madhehebu, wala alikuwa haombi juu ya umoja wa watu wote wa ulimwengu. Yesu alikuwa na mawazo tofauti kwa ajili ya maombi yake.
Narudia tena swali hili; Yesu Kristo alipokuwa anaomba juu ya umoja, alikuwa anaomba kwa ajili ya nani? Kwa sababu Yesu Kristo alifufuka, na yuko hai hata sasa na hata milele, naona ni vizuri tumuulize yeye mwenyewe swali hili.
Je, Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, ulipokuwa unaomba juu ya umoja, ulikuwa unamuombea nani? Tunakuomba tunapolisoma neno lako, Roho wako Mtakatifu atutie nuru katika macho yetu ya kiroho, tupate kuelewa na maandiko.
Yesu Kristo ni Neno (Yohana 1:1-5,14). Kwa hiyo tunapolisoma Neno; tunamsoma Kristo na mawazo yake. Na kwa ajili hiyo, tunapata jibu la swali tulilomuuliza Bwana, kwa kulisoma Neno la Mungu, ambalo ndilo lililobeba mawazo yake.
Yesu aliomba Umoja kwa ajili ya Kanisa.
Napenda kukiri wazi ya kuwa, neno kanisa bado halijaeleweka vizuri kwa watu wengi. Kwa hiyo ninaposema ya kuwa, Yesu aliomba Umoja kwa ajili ya kanisa, nina maana ya kulitumia neno kanisa kama vile linavyotumika na Biblia.
Kanisa maana yake nini?
Kuna mtu mmoja ambaye aliniuliza maswali mbali mbali juu ya mapokeo ya madhehebu ya kikristo, na kwa nini mengi ya mapokeo hayo yanapingana.
Na mimi kabla ya kumjibu nilimuuliza swali hili; “Je, unafahamu tofauti iliyopo katika dhehebu na kanisa?
Akasema ‘ndiyo’.
Nikamuuliza tena; ‘Kanisa ni kitu gani’
Akasema; ‘Kanisa ni jengo ambalo tunakwenda kila Jumapili kusali ndani yake’.
Niliposikia jibu hilo, nilipata mshangao mkubwa sana. Nilipata mshangao si kwa sababu jibu lilikuwa ni sahihi. Hapana! Bali kwa sababu jibu hili lilikuwa si sawa. Na zaidi ya hapo limesemwa na mkristo ambaye nilikuwa naamini anafahamu siku nyingi maana ya Kanisa.
Na ndipo nilipoona umuhimu wa mafundisho kwa wakristo. Ni kweli kabisa watu wa Mungu tunahitaji mafundisho yenye uzima na ya kiroho.
Sijui huyo Ndugu anaposikia watu wakisema tuombe juu ya umoja wa kanisa, alikuwa anaelewa kitu gani!
Je unafikiri Yesu Kristo alikuwa anaomba juu ya umoja wa kanisa lililojengwa kwa mikono ya wanadamu?
Je! Unadhani Yesu Kristo alikuwa anaomba juu ya umoja wa matofali, vyuma, mchanga, mabati, misumari na saruji?
La hasha!
Yesu Kristo alipoomba juu ya umoja, alikuwa haombi juu ya umoja wa jengo tunalokwenda kuabudu ndani yake kila Jumapili au Jumamosi!
Kwa nini?
Kwa sababu, tunaelewa ya kuwa tunapaswa kumwabudu Mungu katika roho na kweli. Imeandikwa hivi:
“Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli”. (Yohana 4:23, 24)
Kwa hiyo, kuwa na jengo la kwenda kuabudu kila Jumapili au Jumamosi haitoshi, kama watu wanaoabudu ndani yake hawatamwabudu Baba katika roho na kweli.
Na tena, ni budi tufahamu ya kuwa Mungu ambaye ni Roho, hakai katika majengo yaliyojengwa kwa mikono ya wanadamu (Matendo ya Mitume 7:47-49; Isaya 66:1)
Mungu ambaye ni Roho, huishi katika jengo ambalo amelijenga mwenyewe kwa mkono wake, tangu Bwana Yesu alipokufa na kufufuka. Na jengo hilo linaitwa kanisa.
Sasa, kanisa ni kitu gani?
Kanisa ni mwili wa Kristo! Na jambo hili limewekwa wazi katika sala hii ya mtume Paulo:
“Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo na utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo, na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadri ya utendaji wa nguvu za uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadri ya utendaji wa nguvu za uweza wake, aliutenda katika Kristo alipomfufua katika watu, akamweka mkono wake wa kiume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akavitia vitu vyote chini ya miguu yake akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya KANISA; ambalo ndilo MWILI WAKE” (Waefeso 1:17-23)
Maneno hayo yanatupa picha na maana nzuri juu ya kanisa, ya kwamba kanisa ni mwili wa Kristo. Na kwamba huo mwili ndio ukamilifu wake Kristo, anayekamilika kwa vyote katika vyote. Maneno hayo pia yanaondoa mawazo ya watu wengi wanaofikiri ya kwamba kanisa ni dhehebu fulani au dhehebu lao ndilo kanisa.
Ngoja nikueleze; kanisa si dhehebu, na dhehebu si kanisa. Nawala hakuna mahali katika biblia panaposema kanisa ni dhehebu na dhehebu ni kanisa. Dhehebu ni dhehebu, na kanisa ni kanisa. Kanisa ni mwili wa Kristo!
Na mwili wa Kristo ni kitu gani?
“Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja…….Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo na viungo kila kimoja peke yake. (1Wakorintho 12:12, 13, 27)
Neno la Mungu linatuambia ya kuwa mwili wa Kristo ni mmoja na kichwa cha mwili huo ni mmoja. Ni muhimu tulijue hili kwa undani ya kuwa hakuna mwili wa Kristo zaidi ya mmoja. Kwa sababu kungekuwa na mwili wa Kristo zaidi ya mmoja, basi ingebidi pia kuwa na kichwa cha mwili zaidi ya kimoja.
Unapowaangalia wakristo ulimwenguni pote, unapata picha ya haraka inayoonyesha ya kuwa Kristo ana miili mingi, au picha inayoonyesha mwili wa Kristo uliogawanyika. Hii ni hali ya kusikitisha sana machoni pa Mungu katika Yesu Kristo, na machoni pa watu wengine.
Yesu Kristo alipokuwa anasema “Nitalijenga kanisa langu….” Hakuwa anamaanisha ya kuwa atalijenga kanisa liwe vipande vipande; na zaidi sana alikuwa hamaanishi kuujenga mwili wake uwe vipande vipande. Yesu Kristo alikusudia na bado amekusudia kulijenga kanisa katika umoja ulio mkamilifu. Amekusudia kuujenga mwili wake katika umoja ambao hauwezi kuharibiwa na wala milango ya kuzimu haitaliweza (Mathayo 16:18).
Sisi sote tuliobatizwa kwa Roho mmoja wa Kristo; sisi sote tuliozaliwa mara ya pili kwa Roho wa Mungu; tumeunganishwa kuwa mwili mmoja wa Kristo. Umoja huu wa Roho wa Kristo ndani ya wanadamu walioamua kumwamini na kumfuata katika roho na kweli haujafungwa na mipaka yoyote ya kibinadamu. Umoja huu wa Roho ya Kristo ndani ya watu haujafungwa na mipaka ya kidhehebu, wala kikabila, wala kitaifa, wala kirangi wala kibiashara, na hata shetani mwenyewe hawezi kuzuia umoja huu!
Kanisa ni mwili wa Kristo. Na mwili wa Kristo ni watu walio zaliwa mara ya pili kwa Roho wa Mungu. Na pia imeandikwa; “Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili, bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake.” (Warumi 8:8)
Watu waliozaliwa mara ya pili mahali popote ulimwenguni ni “Mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.” (1Wakorintho 12:27)
Na kwa sababu hii, naomba Roho wa Mungu akuwezeshe kuliona kanisa kama Neno la Mungu linavyosema. Ondoa mipaka uliyojiwekea juu ya kanisa, lione kanisa katika upana wake, na urefu na kina. Mipaka yote ya kidhehebu, kikabila, kitaifa, kirangi, na ivunjike kwa Jina la Yesu Kristo!
Watu wote waliozaliwa mara ya pili kwa Roho wa Mungu (Yohana 3:1-8) hao ndio mwili wa Kristo. Na kwa maneno mengine wanaitwa, walioongoka, au watu wa Njia hii, au watu wa Kristo, au waliookoka. Na ndiyo maana imeandikwa; “ Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa.” (Matendo ya Mitume 2;47)
Kwa usemi mwingine tunaweza kusema, Bwana akauongeza mwili wake mwenyewe kwa wale waliokuwa wakiokolewa!
Kumbuka pia ya kuwa imeandikwa; “Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili, na kilichozaliwa kwa Roho ni Roho.” (Yohana 3:6) na Kristo ni Neno, na Neno ni Mungu, na Mungu ni Roho, kwa hiyo Kristo ni Roho. Ikiwa Kristo ni Roho basi na mwili wake ni roho kuwa umezaliwa kwa Roho.
Na ni kweli kwamba si wote wanaoitwa wakristo siku hizi wamezaliwa mara ya pili kwa Roho wa Kristo. Na kwa ajili hii, si wote wanaoitwa wakristo siku hizi ambao ni viungo vya mwili wa Kristo.
Yesu Kristo alipokuwa anaomba juu ya umoja alikuwa anaomba juu ya umoja wa rohoni wa nia za watu waliozaliwa mara ya pili kwa Neno. (1Petro 1:23) kwa kuwa Neno ni Roho. (Yohana 6:63)
Yesu Kristo alipokuwa anaomba umoja alisema:
“Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu waliokuwa wako, ukanipa mimi, na neno lako wamelishika. Sasa wamejua ya kuwa yote uliyonipa yatoka kwako. Kwa kuwa maneno uliyonipa nimewapa wao; nao wakayapokea, wakajua hakika ya kuwa nalitoka kwako, wakasadiki ya kwamba wewe ndiye uliyenituma. Mimi nawaombea hao; SIUOMBEI ULIMWENGU; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako, na wote walio wangu ni wako, na walio wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao….Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao.” (Yohana 17:6-10, 20)
Kwa maandiko hayo machache tunaweza kuona ya kuwa maombi ya Yesu juu ya Umoja yalikuwa yamelenga na kukusudiwa kwa ajili ya kundi la watu waliolishika neno lake, na neno hilo likawafanya wazaliwe mara ya pili (1Petro 1:23), na kuitwa viungo vya mwili wa Kristo, ambalo ndilo Kanisa, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote. (Waefeso 1:22,23, Warumi 12:4,5)
Pia, unaweza kuona ya kuwa Yesu Kristo alipoomba juu ya umoja wa Kanisa, alikuwa na mawazo tofauti sana na watu wengi siku hizi wanaoomba juu ya umoja wa kanisa. Watu wengi wanapoomba juu ya umoja wa kanisa, huwa wana maana ya kuomba juu ya umoja wa dhehebu lao. Na hii inatokana na kulielewa neno kanisa kuwa lina maanisha dhehebu lao.
Lakini Kanisa si dhehebu; na dhehebu si kanisa. Yesu alipokuwa anaomba umoja alikuwa haombi juu ya umoja wa dhehebu lolote lile. Yesu Kristo alipokuwa anaomba umoja, alikuwa anaomba umoja wa roho za watu waliolipokea neno lake liletao wokovu, na kuwawezesha kuzaliwa mara ya pili, walio ulimwenguni pote, NDANI na NJE ya madhehebu mbalimbali.
Kwa kusema hivi HAIMAANISHI ya kuwa kuomba kwa ajili ya dhehebu lako ni vibaya. La hasha! Tafadhali ISIELEWEKE HIVYO. Ukitaka kuomba juu ya umoja wa dhehebu lako, omba hakuna mtu anayekuzuia.
Lakini nasema na dhamiri yangu ikinishuhudia katika Roho Mtakatifu ya kuwa, maombi ya Yesu juu ya umoja yaliyoandikwa katika kitabu cha Yohana Mtakatifu sura ya 17, yalikuwa ni kwa ajili ya watu waliozaliwa mara ya pili kwa Roho, ambao wanaweza kuwa ndani ya dhehebu, na nje ya dhehebu. Kwa kuwa wokovu haukuletwa na dhehebu lolote na kwa hiyo hakuna dhehebu linaloweza kudai ya kuwa ndilo chanzo cha wokovu.
Kwa kuwa imeandikwa:“Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao Wokovu, kwa KILA aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia.” (Warumi 1:16)
Wokovu unaletwa na uweza wa Mungu, ambao ndiyo Injili au habari Njema zilizoletwa na Yesu kwa watu wote. Yesu Kristo ndiye Injili ya kweli, kwa maana yeye ndiye habari njema kwa watu wote. Kwa Yesu Kristo tunapata wokovu. Palipo na Yesu Kristo, pana wokovu wa kweli. Huwezi ukampenda Yesu Kristo na ukaukataa wokovu na kuuchukia – huo ni unafiki.
Huwezi ukamtenga Yesu Kristo na wokovu aliouleta. Ukimpenda Yesu Kristo, penda na habari za wokovu alizoleta. Ukimpokea Yesu Kristo, pokea na wokovu aliouleta kwa njia ya msalaba na kufufuka kwake.
Basi, fahamu kuanzia sasa, kama ulikuwa hujafahamu ya kuwa, wokovu haukuletwa na dhehebu, bali na Injili iliyo hai, inayohubiriwa na watu waliozaliwa mara ya pili kwa Roho Mungu, waliomo NDANI na NJE ya madhehebu unayoyafahamu na usiyoyafahamu.
Ikiwa dhehebu si kanisa, dhehebu ni nini?
Hili ni swali zuri kabisa ambalo inabidi tujiulize.Ikiwa dhehebu si kanisa, na kanisa si dhehebu, basi dhehebu ni kitu gani?
Mimi mwenyewe nimekuwa nikijiuliza swali hili muhimu, tangu nilipofahamu maana halisi ya kanisa, kama neno la Mungu linavyotuambia. Mchungaji mmoja wa siku nyingi, aliwahi kuniambia kuwa madhehebu mbali mbali ya kikristo ulimwenguni ni viungo mbali mbali vya mwili wa Kristo.
Ukiangalia jambo hili kijuu-juu tu, unaweza ukakubaliana na usemi wa mchungaji huyo. Lakini ukilichunguza jambo hili kwa “jicho” la Neno la Mungu utaona ya kwamba usemi huo si sahihi hata kidogo.
Nilipousikia usemi huo kwa mara ya kwanza, ulinifanya nianze kuiangalia biblia kwa undani zaidi, ili niweze kupata ukweli wa maana ya kanisa na dhehebu, na uhusiano uliopo katikati yao.
Nilianza na Neno kanisa, kwa kusoma na kutafakari kila mahali katika biblia palipoandikwa kanisa au makanisa. Na nikakuta ya kwamba neno kanisa au makanisa limetokea katika biblia kwa mara zisizopungua tisini na tisa. Na maana ya Kanisa ni mwili wa Kristo. (Waefeso 1:22,23) na mwili wa Kristo ni muunganiko wa roho za watu waliozaliwa mara ya pili kwa Roho wa Mungu popote walipo ulimwenguni (1Wakorintho 12:12-27; Warumi 12:4-21; Yohana 3:1-21, Matendo ya Mitume 2:37-47).
Hakuna mahali ambapo nilikuta pameandikwa ndani ya biblia ya kuwa madhehebu ni viungo vya kanisa, au pameandikwa ya kuwa dhehebu ni kanisa au kanisa ni dhehebu. Kwa sababu hii, hamu yangu ilizidi sana ya kutaka kujua biblia inasema nini juu ya madhehebu.
Kwa hiyo nilianza kusoma na kutafakari kila mahali katika biblia nilipokuta pameandikwa neno dhehebu au madhehebu. Na ninakuta ya kwamba neno dhehebu au madhehebu limetokea katika biblia kwa mara tano hivi.
Na nilikuta ya kuwa madhehebu yalikuwepo hata KABLA ya Yesu Kristo kuzaliwa na bikira Maria, kama Mwana wa Mungu.
Biblia inazungumza juu ya “Madhehebu ya masadukayo” (Matendo ya Mitume 15:5)
Madhehebu haya yalikuwepo tangu kabla Yesu Kristo hajazaliwa duniani kama Mwana wa Mungu na Mwana wa Adamu. Na alipokuwa duniani katika maisha yake ya mwanzo alilelewa katika namna na jinsi madhehebu hayo yalivyokuwa yanamwabudu Mungu. Alitahiriwa siku ya nane kama ilivyokuwa desturi ya wayahudi na madhehebu hayo. Na wazazi wake wakamtolea sadaka kama ilivyokuwa desturi yao katika kufuata torati ya Musa (Luka 2:21-24)
Madhehebu hayo ya Mafarisayo na Masadukayo yalikuwa yanamwamini Mungu wa Israeli, ambaye pia ni Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, na ni Baba yetu sisi. Na madhehebu ya kikristo yanamwamini Mungu huyo huyo.
Lakini Yesu Kristo alipoanza kuhubiri juu ya habari njema za Ufalme wa Mbinguni uletao wokovu, walidhani analeta machafuko kati yao, wakamshitaki, wakamsulubisha na wakamuua. Lakini siku ya tatu akafufuka kutoka katika wafu, na mpaka leo yupo hai, akiwa ndiye tumaini letu la uzima wa sasa na wa baadaye.
Ingawa madhehebu hayo yalikuwa yanamwamini Mungu mmoja na kutumia wote torati hiyo hiyo ya Musa, yalikuwa yanatofautiana katika mapokeo yao. Hebu soma na kutafakari habari hii:
“Paulo alipotambua ya kuwa sehemu moja ni Masadukayo, na sehemu ya pili ni Mafarisayo, akapaza sauti yake katika ile baraza, Ndugu zangu, mimi ni Farisayo, mwana wa Farisayo; Mimi ninahukumiwa kwa ajili ya tumaini la ufufuo wa wafu. Alipokwisha kunena hayo palikuwa na mashindino baina ya Mafarisayo na Masadukayo, mkutano ukafarakana. Kwa maana Masadukayo husema ya kwamba hakuna kiyama wala malaika wala roho; bali Mafarisayo hukiri yote.” (Matendo ya Mitume 23:6-8)
Tunaona ya kuwa mkutano huu uliokusanyika ili kumhukumu Paulo, ulifarakana kwa sababu ya tofauti za mapokeo ya madhehebu yao. Hata hivi leo mahali pengi wakristo wamefarakana kwa sababu ya tofauti za mapokeo ya madhehebu yao. Hili ni jambo la kushangaza kwa sababu, madhehebu hayo ya kikristo, yote yanakiri kumhubiri Kristo, na kumwamini Mungu mmoja katika yeye.
Lakini swali linajitokeza hapa nalo ni hili; Je! Kristo akihubiriwa huwa anawafarakanisha watu na kuwatawanya, au huwa anavuta WOTE kwake? Soma Yohana 12:32 imeandikwa:-
“Nami (Yesu) nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu.”
Ikiwa ni hivyo basi, ni Yesu yupi anayehubiriwa siku hizi ambaye anatawanya watu?
Ni kweli kwamba Neno la Mungu lililetwa na Yesu, linamwondoa mtu toka Ufalme wa giza na kumwingiza katika Ufalme wa Mungu (Wakolosai 1:13). Na pia neno la Mungu linamtenga mtu na tamaa za dunia.
Lakini pia Neno lenye pumzi ya Mungu limewekwa ili kuwaunganisha watu wa aina mbali mbali pamoja na Mungu katika roho na kweli, kwa njia ya damu na ufufuo wa Yesu Kristo!
Na nilipoendelea kuisoma, nilishangaa kuona kwamba biblia, haitumii maana ya neno dhehebu moja kwa moja na iliyo wazi kama vile ilivyofanya kwenye maana ya kanisa. Neno dhehebu limetumika katika misingi ambayo wasomaji wanatarijiwa wawe wanafahamu maana yake.
Kwa hiyo niliposoma maana ya neno dhehebu kama ilivyotolewa na kamusi mbali mbali za maneno, niliona zimelieleza neno dhehebu sawa sawa na jinsi lilivyotumika katika biblia, na jinsi linavyotumika hivi leo.
Dhehebu ni jamii ya watu waliokubaliana wao wenyewe kufuata utaratibu wa aina fulani katika kumwabudu Mungu, ambao wao wanauona ni bora zaidi kuliko wa dhehebu jingine. Hii ndiyo maana kila dhehebu linavutia kwake katika kuzungumza na watu juu ya kumwabudu Mungu.
Na wadhehebu ya Kikristo ni mengi, na ya taratibu zinazotofautiana za kumwabudu Mungu. Na kila dhehebu linaona utaratibu wake wa kuabudu ni mzuri kuliko wa dhehebu jingine. Na kwa sababu hii kuna faraka kati ya wakristo wa madhehebu mbali mbali.
Tangu siku nyingi sana ulimwengu kuna madhehebu ya aina mbali mbali. Kuna madhehebu ya kikristo, ya kiislamu, ya kihindi, na kadhalika. Madhehebu yote hayo yana taratibu zao za kumwabudu Mungu, ambazo zinatofautiana.
Lakini namshukuru Mungu, kwa kuwa ukristo si dhehebu. Ukristo ni maisha ya Mungu yaliyodhihirishwa ndani ya Kristo, anayekaa ndani ya watu. Ukristo ni tabia ya Kristo. Mtu anakuwa mkristo, kwa kuwa anaonyesha tabia ya Kristo katika maisha yake, kwa kuongozwa na Roho wa Kristo.
Ndiyo maana imeandikwa, “Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake”. (Warumi 8:9b)
Wakristo wa kweli, walio na Roho wa Kristo, hao ndio Kanisa yaani mwili wa Kristo.
Ukristo si dhehebu, na kanisa si dhehebu. Umoja wa kanisa si umoja wa madhehebu. Umoja wa kanisa upo na umoja wa madhehebu upo.
Neno la Mungu linatuambia ya kuwa mwili wa Kristo ni mmoja (1Wakorintho 12:20). Kwa hiyo kanisa ni moja tu ulimwengu pote.
Hakuna kanisa zaidi ya moja ambalo ni mwili wa Kristo. Lakini madhehebu ni mengi sana duniani.
Je! bado una mawazo ya kuwa madhehebu ni viungo mbalimbali vya Kanisa? Watu wengi wana mawazo ya namna hii. Lakini biblia haisemi hivi:
“Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo na viungo kila kimoja peke yake.”
Neno halisemi kuwa; “Basi madhehebu yamekuwa mwili wa Kristo ni viungo kila kimoja peke yake.”
Neno linasema kuwa; “ Basi NINYI mmekuwa mwili wa Kristo na viungo kila kimoja peke yake.”
Ni kweli kwamba kuna WATU walio viungo vya mwili wa Kristo walio ndani ya madhehebu mbali-mbali ya kikristo. Lakini madhehebu yenyewe si viungo vya mwili wa Kristo.
Kwa nini naeleza haya?
Ni kwa kuwa kama tusipofahamu tofauti na uhusiano uliopo kati ya kanisa na dhehebu; basi haitakuwa rahisi kwetu kufahamu sababu zilizomfanya Yesu Kristo atuombee umoja.
Kwa sababu ya kutokufahamu uhusiano huo, watu wengi wamekuwa wakiomba juu ya umoja wa madhehebu WAKIDHANI wanaomba juu ya umoja wa kanisa. Na kwa sababu hii maombi hayo hayajajibiwa, kwa kuwa wanaomba umoja ili wautumie kwa tamaa zao. (Yakobo 4:1-3)
Ni kweli pia kuwa katika siku za mwisho kutatokea umoja wa madhehebu kama ilivyotabiriwa. Lakini hatutalijadili suala hili katika somo hili.
Lakini nina uhakika ya kwamba watu wengi wanataka na wanapenda kuwe na umoja katika mwili wa Kristo. NA NDILO LILILOKUWA LENGO LA KRISTO KATIKA KUTUOMBEA UMOJA.
Na katika madhehebu ya Kikristo, kila moja limeanzishwa kwa kutumia mistari michache katika biblia. Na ili mtu aweze kuruhusiwa kushiriki katika dhehebu fulani ni sharti kwanza atimize masharti ya dhehebu hilo analotaka kuingia.
Na kuingia katika mwili wa Kristo kuna masharti yake ambayo ni kuzaliwa upya mara ya pili na Roho Mtakatifu. (1Wakorintho 12:13, Yohana 3:5) Lakini katika madhehebu utakuta watu wa aina mbili kubwa; waliozaliwa mara ya pili kwa Roho wa Mungu na ambao bado hawajazaliwa mara ya pili kwa Roho Mungu. Yesu Kristo alipokuwa anaomba juu ya umoja alikuwa anaomba kwa ajili ya wale tu waliozaliwa mara ya pili kwa Roho wake na watakaozaliwa baadaye kabla ya yeye kurudi mara ya pili kulichukua kanisa.
Ninapoyasema haya simaanishi ya kuwa uyachukie madhehebu, bali ufahamu tofauti iliyopo kati yake na kanisa. Na kwamba kukubaliwa na dhehebu fulani haitoshi kukurithisha ufalme wa Mungu, BILA ya kuzaliwa mara ya pili kwa Roho wa Mungu.
BILA kumpokea Kristo moyoni mwako na kuwa mwana wa Mungu (Yohana 1:12) kuwa mkristo wa dhehebu tu hakutatosha kitu.
Hii ni kweli kabisa!
Biblia inazungumzia juu ya “madhehebu ya Masadukayo” (Matendo ya Mitume 5:17) Na pia Biblia inazungumza juu “Madhehebu ya Mafarisayo” (Matendo ya Mitume 15:5)
Hayo madhehebu yalikuwepo hata kabla ya Yesu kuzaliwa. Yesu Kristo alipotembea juu ya nchi alikutana nayo. Na fahamu ya kuwa viongozi wa madhehebu ndio waliomsulubisha Yesu Kristo. Sasa nauliza swali: Ikiwa Mungu aliona ya kuwa madhehebu yanatosha kumpatanisha yeye na mtu, kwa nini basi alimtuma Yesu Kristo, Mwana wake afe kwa ajili yetu?
Mungu alikuwa na sababu muhimu kabisa. Mungu alijua kabisa kuwa taratibu za madhehebu haziwezi kuleta ondoleo la dhambi.
Mungu alijua kabisa kuwa taratibu za madhehebu haziwezi kumpa mtu uzima wa milele. Kwa hiyo ilibidi Yesu Kristo aje azaliwe, afe na afufuke ili kila amwaminiye apate ondoleo la dhambi na uzima wa milele. (Yohana 3:16-18).
Tufanyeje basi ndugu zangu?
Ninapoyaandika yote haya sina nia mbaya na mtu yeyote. Lakini moyo wangu unapata uchungu mkali ninapoona watu wengi waliookoka hawapatani na viongozi wa madhehebu mbalimbali ya kikristo.
Hali ya vikundi mbali mbali vya uamsho, vimekuwa na mawazo ambayo si mazuri juu ya viongozi wa madhehebu hasa ambao hawajaokoka na wanapinga wokovu. Na kwa sababu hii viongozi wa madhehebu wanakuwa na wasiwasi na watu waliookoka na hili si kosa lao ni letu! Hatuenendi sawa sawa na Neno la Mungu mara nyingi!
Swali ninalotaka kulisema hapa ni uhusiano kati ya wakristo na madhehebu yao au uhusiano wa kanisa na madhehebu, au uhusiano wa watu waliookoka na madhehebu.
Kuna sehemu zingine ambazo imefikia hali ambayo mtu akiokoka hataki tena kwenda kwenye nyumba za ibada. Je! hii ni busara ya Mungu Na badala yake masengenyo na manung’uniko yanazidi kuwasema viongozi fulani. Je! hii ni sawa?
Kumbuka Yesu alitembea duniani sawa sawa na wewe; lakini biblia inasema alizidi kila wakati kumpendeza Mungu na wanadamu
“Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.” (Luka 2:52)
Na fahamu ya kuwa wanadamu ambao aliwapendeza Yesu, walikuwepo viongozi wa madhehebu na watu wa kawaida, ambao wote walikuwa hawajaokoka. Sasa mbona watu waliookoka wengi wanashindwa na hili wakati imewapasa kuenenda sawasawa na Yesu alivyoenenda? (1Yohana 2:6)
Unaweza kusema, mbona basi hao wanadamu walimsulubisha Yesu? Hili ni swali zuri lakini kumbuka Yesu hakutafuta kuwakimbia kwa kuwa aliwapenda upeo (Yohana 13:1) , ingawa watu fulani walimchukia.
Jambo ninalotaka kusema hapa ni kwamba si vizuri na si hekima na si mpango wa Mungu kumchukia mtu na kumnenea vibaya kwa sababu tu ya msimamo wake juu ya wokovu. Kumbuka tumeamriwa kuwapenda majirani zetu (watu wanaotuzunguka) kama nafsi zetu wenyewe, HATA kama hawajaokoka.
Watu wakikuchukia wewe kwa kuwa umeokoka au umekuwa mkristo, wewe wapende. Hebu soma maneno haya ya Yesu kwa watu wake:
“Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua waovu na wema huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, Je! nao hawafanyi yayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa Mataifa, Je? nao hawafanyi kama hayo? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mathayo 5:43-48)
Na tuone pia jinsi ambavyo Mtume Paulo alivyofanya aliposhitakiwa na viongozi wa madhehebu wa wakati ule, kwani walifikiri Paulo analihubiri dhehebu jipya liitwalo “dhehebu la wanazarayo” kwa kuwa alimhubiri Yesu wa Nazareti. (Matendo ya Mitume 24:5)
Wakati Kuhani Anania alipoamuru Paulo apigwe; Paulo alimtukana Mkuu huyo akisema, “Mungu atakupiga wewe, ukuta uliopakwa chokaa”(Matendo ya Mitume 23:2-3)
“Wale waliosimama karibu wakasema, Je! unamtukana Kuhani Mkuu wa Mungu? Paulo akasema, Sikujua, ndugu zangu, ya kuwa yeye ni Kuhani Mkuu, maana imeandikwa, Usimnenee mabaya Mkuu wa watu wako”. (Matendo ya Mitume 23:4-5)
Ingawa Mtume Paulo alifahamu kabisa ya kuwa Kuhani Mkuu huyo alikuwa hajaokoka lakini ilibidi awe mtendaji wa neno la Mungu, na akamheshimu kwa kuwa imeandikwa, usimnenee mabaya mkuu wa watu wako.
Hili ni fundisho hata kwetu hivi leo, inatubidi tuwe watendaji wa Neno la Mungu, tusiwanenee vibaya viongozi wa madhehebu ambao hawajaokoka kwa kuwa imeandikwa, Usimnenee mabaya mkuu wa watu wako. Na pia tutafute kwa bidii kuwa na amani na watu wote.
Pia Soma Warumi 13:1-10 juu ya kutii wenye mamlaka. Mstari ule wa saba unasema, “ Wapeni wote haki zao; mtu wa kodi, kodi, mtu wa ushuru, ushuru, astahiliye hofu, hofu; astahiliye heshima, heshima”
Posted by Strictly Gospel 






















