Binadamu/Mtu ameumbwa akiwa na muungano wa MWILI, NAFSI na ROHO. Vitu hivi vitatu ni picha au mfano wa Utatu Mtakatifu wa Mungu. Utatu Mtakatifu ni kitu Kimoja. Wameungana. Hufanya kazi pamoja!
Yohana 14:10 “Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake.”
Yohana 15:26 “Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia.”
Maandiko hayo mawili hapo juu yanaonyesha UMOJA wa UTATU huo.
Utatu wa Mtu, kama ilivyoandikwa pale mwanzoni, unatengenezwa na MWILI,NAFSI na ROHO. Tatizo lililopo hapa ni kwamba Utatu huu siyo mara zote unafanya kazi kwa pamoja! Siyo wakati wote vitu hivi vitatu huwa vinatembea pamoja. Kuna wakati Mwili unaweza kuwa sehemu moja lakini Nafsi iko sehemu nyingine! Ndiyo maana inawezekana mtu akawa, mfano, Kanisani lakini Mawazo/Nafsi iko mahali kwingine, akiwaza mengine tofauti kabisa na kile mwili unafanya pale kanisani! Bwana Yesu analijua hili ndiyo maana anasema, katika Mathayo 15:8, kwamba “Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami.”
Tena, wakati UTATU Mtakatifu hufanya kazi pamoja, lakini UTATU wa Mtu HUSHINDANA: Wagalatia 5:17 “Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka.”
Yako maandiko mengi yanayoonyesha kwamba kuna Mgogoro ndani ya Mtu. Twaweza kumuona mtu anacheka, uso wake umejaa tabasamu lakini moyoni ana majonzi! Twaweza kumuona mtu anaimba na kucheza lakini kumbe mawazo yake yako mbali. Kwa wakati wako unaweza kusoma maandiko yafuatayo ili kuona jinsi kulivyo na mgogoro katika Utatu wa Mtu: Marko 9:47, Yeremia 17:9, Wagalatia 5:19-22)
Mtu Akimpokea Yesu na Kukubali kuishi maisha ya Kumcha Mungu, Mfarakano kati ya Mwili, Nafsi na Roho HUONDOLEWA. Huwa panatengenezwa Muungano unaoanzia Rohoni na kuishia Mwilini. Mtu aliyeokoka na Kujazwa na Roho Mtakatifu anao UWEZO wa Kuvitiisha Nafsi na Roho yake. Ndipo Neno la Mungu linasema, katika Wagalatia 5:16 “Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili.” Huu ndio Uelekeo Sahihi wa Utawala ndani ya Mtu ili Utatu wake uwe na UMOJA. Haiwezekani kuwa na Umoja katika Utatu wa Mtu kwa Kuufanya MWILI NDIO UWE KIONGOZI “kwa maana kama mkiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. (Warumi 8 :13). Na tena katika Wagalatia 5:19-22 yameorodheshwa mambo ambayo Mwili ukipewa Ungozi ndiyo yatapewa Msisitizo wa kwanza!
Mtu ambaye Utatu wake Umefarakana Ni rahisi tuu KUSEMA UONGO kwa kuwa ndani yake HAKUNA UMOJA. Twaweza kuona mfano mmoja ambao ni KUAPISHWA KWA WABUNGE NA VIONGOZI MBALIMBALI. Watu hawa Huapa wakiwa wameshikilia Vitabu Vya Dini, kwa kuamini kwamba wanayoyatamka hapo ni ya kweli. Lakini utashangaa mtu akiingia kazini na kupewa Ofisi Anayotenda ni tofauti kabisa na vie alivyoapa!! Hii ni kwa sababu aliapa kwa mdomo tuu lakini Moyo wake haukuambatana na Maneno aliyokuwa akiyatamka!
Mtu aliyezaliwa mara ya pili ni Mkweli. Hawezi kusema Uongo maana akitaka kudanganya Roho yake hukataa. Mtu akifika katika kiwango hicho ” Ndiyo” yake inakuwa ni “Ndiyo” na “Hapana” inakuwa ni “Hapana”. (Mathayo 5:37 “Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.”)
Hasara za UTATU ULIOFARAKANA
Mtu ambaye Hana Umoja katika Nafsi yake:
-Ni Muoga,
-Hana amani,
-Hana Furaha ya kweli,
-Hana ujasiri wa kwenda mbele za Mungu kwa maana Anapopiga magoti kumuomba Mungu mashitaka ya maovu huanza kutangulia ndipo maombi yake yanafuata nyuma! (1Yohn 3:21).
-Hawezi kuwa na Uhakika kama kweli Mungu kasikia maombi yake.
-Ni mtu wa kujihukumu mbele za Mungu.
-Hana Ujasiri wa Kumkiri Yesu mbele za Watu!
-Hawezi kukubali kosa hata kama anajua kabisa ametenda bali hutafuta sababu za uongo ili kutetea uongo wake.
Hakuna Amani kubwa kwa mtu zaidi ya ile Ipatikanayo kwa Kufanywa Upya kwa Kuzaliwa Mara ya pili na Roho ndiyo ikachukua Usukani wa Uongozi. Mtu anakuwa ni mkweli. Yuko huru mbele za Mungu na Watu. Hata akiitwa Kufa hana wasiwasi kwa kuwa Roho yake hushuhudia kwamba ni mtenda mema; ni mcha Mungu wa kweli.
Jichunguze mwenyewe kwa maana Shahidi wa mambo ya mtu ni mtu mwenyewe!